Poems

Mkata wa maneno

Zacheka nami zangu chekeo
               zacheka zafurahika
Sina mawazo    kichwani leo
               Bado hayajarauka ...
 
Nadhani ni asubuhi
               imeanza kuchipuka
Nayo ndiyo sababu
               ya moyo kuliwazika
na huu mdundo mtamu
               mwema ulotandazika
 
Najichekea ... kwani najua vyema
kwamba sijazoea hali hii tabasama
ijitembezayo kwa shairi na kwa ngoma
ikichezacheza nami ... ikininyegeza kama mke na mume
                                                          kama wapenzi daima
 
Najua sijaizoea hali hii ya furaha na shauku
                ijigambayo kwa mchana na usiku
                kufuata mtindo wa manju kila siku
                ... kufuata anasa za dunia
 
Ndipo nikawa mkata...
              mkata wa maneno ya furaha na amani
                                            ya mahaba au dini
maneno ya kufifisha kisasi cha mja
                juu ya maisha duniani
                maneno ya kushinda vita vya nyoyoni
                hivyo vita vya ndani kwa ndani.
 
Neno langu ni maumivu tu, ni mashaka
Ndipo kapendelea mwenendo wa kale ...
                                                                 fikira kutoziandika.